Nimesikitishwa sana na vitendo vya kihuni vilionyeshwa na wachezaji na baadhi ya wapenzi wa Simba jana pale Neshno.
Simba wanastahili adhabu ikiwemo kufidia uharibu ule wa viti vya kukalia. Na adhabu hiyo isichelewe...
Maggid.

haya ni mabomu ya machozi ambayo yalirushwa ili kudhibiti vurugu hizo
Na Mahmoud Zubeiry, Dar es Salaam
UWANJA wa Taifa, Dar es Salaam jana uligeuka eneo la vita baina ya Polisi mashabiki wa Simba SC, kufuatia Kagera Sugar kupata bao la kusawazisha dakika ya pili ya muda wa nyongeza baada ya kutimia kwa dakika 90 za mchezo wa Ligi Kuu ya Vodacom Tanzania Bara, timu hizo zikitoka 1-1.
Baada ya Salum Kanoni kukwamisha nyavuni mkwaju wake wa penalti, mashabiki wa Simba waliokuwa viti vya Rangi ya Bluu na Chungwa, walianza kung'oa viti na kuvitupia uwanjani.

hapa mashabiki wakikimbia baada ya vurugu hizo kuanza kutokea na mabomu kuanza kurushwa

Mara moja, Polisi walianza kupambana na mashabiki hao kwa kuwatupia mabomu ya machozi, ndipo wakaanza kukimbia. Makocha na wachezaji wa Simba kwa pamoja waliwafuata waamuzi kuwalalamikia- hali ambayo ilifanya watolewe kwa kusindikizwa na Polisi.
Katika mchezo huo, uliochezeshwa na refa Mohamed Theofile wa Morogoro aliyesaidiwa na Said Mnonga na Charles Chambea wote wa Mtwara, ambao walishindwa kuumudu kabisa, hadi mapumziko, Simba SC walikuwa mbele kwa bao 1-0.

hivi ni baadhi ya viti vilivyong'olewa na mashabiki
Bao hilo lilifungwa na mshambuliaji wa kimataifa wa Burundi, Amisi Tambwe dakika ya 45 baada ya kupokea pasi nzuri ya Betram Mombeki na kumpiga chenga beki Salum Kanoni, kabla ya kumchambua kipa Hannington Kalyesebula.