Pages

ELIMU KWANZA.

ELIMU KWANZA.
FEDHA SIO KIPAUMBELE CHETU.

Wednesday 9 April 2014

BAYERN MUNICH YAING'OA MAN UNITED, BARCELONA NAYO YATUPWA HUKO KWA WASIOJUA

MANCHESTER United ya England imeaga Ligi ya Mabingwa Ulaya baada ya kufungwa mabao 3-1 na wenyeji Bayern Munich Uwanja wa Allianz-Arena mjini Munich, Ujerumani usiku huu.
Hiyo inamaanisha United imeaga kwa kipigo cha jumla ya mabao 4-2, baada ya awali kulazimishwa sare ya kufungana bao 1-1 Uwanja wa Old Trafford mjini Manchester.
United leo ndiyo waliokuwa wa kwanza kupata bao dakika ya 57, mfungaji beki wake Mfaransa, Patrice Evra aliyefumua shuti kali kwa guu la kushoto baada ya kupokea pasi ya Antonio Valencia.


Sekunde 22 baadaye Mcroatia Mario Mandzukic akaisawazishia Bayern akitumia fursa ya wachezaji wa United kuzubaa kwa furaha ya bao, wakidhani biashara imekwisha na kumbe mpira ni hadi filimbi ya mwisho.Bao hilo liliwaondoa mchezoni United na kuanza kufanya madudu, hali ambayo iliwapa fursa mabingwa hao wa Ulaya kupata mabao mawili zaidi.
Tomas Muller alifunga la pili dakika ya 68 pasi ya Arjen Robben ambaye alikuwa mwiba mchungu kwa Mashetani hao Wekundu usiku huu.
Arjen Robben akafunga mwenyewe bao la tatu kwa shuti la mbali dakika ya 76 na kuzima kabisa ndoto za kocha David Moyes kufanya maajabu kwenye michuano hiyo ya Ulaya.


Katika mchezo mwingine, Barcelona imefungishwa virago na Atletico Madrid, zote za Hispania baada ya kufungwa bao 1-0 Uwanja wa Vicente Calderon mjini Madrid, Hispania.
Hiyo inamaanisha Barca imeaga kwa kipigo cha jumla cha mabao 2-1 baada ya awali kulazimishwa sare ya 1-1 Uwanja wa Camp Nou, Barcelona.
Bao lililoizamisha Barca leo limefungwa na Jorge Resurrecion Merodio Koke dakika ya tano akimalizia pasi ya Adrian.
Bayern na Atletico zinaungana na Chelsea ya England iliyoitoa PSG ya Ufaransa na Real Madrid ya Hispania iliyoing’oa Borrussia Dortmund jana kutinga Nusu Fainali, ambayo droo yake itapangwa Ijumaa.

No comments:

Post a Comment