Pages

ELIMU KWANZA.

ELIMU KWANZA.
FEDHA SIO KIPAUMBELE CHETU.

Saturday, 10 May 2014

YANGA WATAKIWA KIGALI KABLA YA AGOSTI 9 KOMBE LA KAGAME

Na Baby Akwitende, Dar es Salaam
MASHINDANO ya Klabu Bingwa Afrika Mashariki na Kati maarufu Kombe la Kagame yamepangwa kufanyika kuanzia Agosti 9 hadi 23 mwaka huu jijini Kigali nchini Rwanda.
Tanzania Bara itawakilishwa na Yanga katika mashindano hayo yanayoandaliwa na Shirikisho la Soka Afrika Mashariki na Kati ( CECAFA).
Akizungumza na BIN ZUBEIRY jana , Katibu Mkuu wa CECAFA, Nicholas Musonye, alisema timu zote wanachama wa shirikisho hilo zinatarajiwa kushiriki.

Kikosi cha Yanga SC

Musonye alisema kuwa bado sekretarieti haijateua timu mwalikwa katika mashindano hayo kutokana na mabadiliko ya kalenda ya michuano hiyo ambayo hufanyika kila mwaka kati ya mwezi Mei na Juni.
"Ratiba kamili ya mashindano hayo itatolewa baadaye", alisema Musonye.
Mlezi wa CECAFA na Rais wa Rwanda, Paul Kagame, ameshathibitisha kutoa zawadiambayo ni Dola za Marekani 60,000 ambazo alianza kutoa tangu mwaka 2002.
Wadhamini wengine waliothibitisha kudhamini mashindano ya mwaka huu ni kituo cha televisheni cha Super Sport.

Bingwa mtetezi wa mashindano hayo ni Atraco ya Burundi na mfungaji bora wa michuano hiyo alikuwa ni Amissi Tambwe, anayeichezea Simba akitokea kwa mabingwa hao.

Thursday, 1 May 2014

TFF YATEUA WAKILI KUCHUNGUZA USAJILI WA DOMAYO AZAM FC

Na Waandishi Wetu, Dar es Salaam
KUTOKANA na tukio lililotokea jana (Aprili 30 mwaka huu) kwenye kambi ya timu ya Taifa (Taifa Stars) iliyopo Tukuyu mkoani Mbeya likihusisha usajili wa baadhi ya timu, Rais wa Shirikisho la Soka Tanzania (TFF), Jamal Malinzi amemteua Wakili Wilson Ogunde kuchunguza mlolongo mzima wa tukio hilo.
Taarifa ya TFF kwa BIN ZUBEIRY leo asubuhi imesema kwamba, baada ya kukamilisha uchunguzi wake, Wakili Ogunde ataishauri TFF kuhusu hatua za kisheria na kikanuni za kuchukua.

Frank Domayo akisaini Azam FC jana
TFF imesema katika taarifa yake inatoa wito kwa wachezaji, klabu na wadau wa mpira wa miguu kufuata kanuni na taratibu katika utendaji wao.
Viongozi wa Azam FC jana walikwenda kwenye kambi ya Taifa Stars kukamilisha taratibu za usajili na kiungo Frank Domayo, aliyemaliza Mkataba wake Yanga SC.
Baada ya kufanikiwa kumsainisha Mkataba wa miaka miwili, wasimamizi wa kambi waliwaitia Polisi viongozi wa Azam FC ambao hata hivyo baadaye waliachiwa. Lakini inadaiwa fomu za usajili zilichanwa.
Azam si klabu ya kwanza kusajili mchezaji katika kambi ya timu ya taifa, kwani vigogo wa soka nchini, Simba na Yanga ndiyo waasisi wa mchezo huo.
Mwaka jana Simba SC walisaini Mkataba mpya na kiungo wao, Amri Kiemba akiwa katika kambi ya Taifa Stars, hoteli ya Tansoma mjini Dar es Salaam.

Inaruhusiwa kwa wakubwa tu; Kiongozi wa Yanga SC, Seif Ahmed 'Magari' alimtoa kambi ya Taifa Stars, beki Kevin Yondan akiwa Simba SC na kumsainisha mwaka 2012.

Yanga SC iliwasajili Domayo kutoka JKT Ruvu, Kevin Yondan kutoka Simba SC wote wakiwa katika kambi ya Taifa Stars Dar es Salaam miaka miwili iliyopita.

CHELSEA NJE ULAYA, YAPIGWA 3-1 DARAJANI...FAINALI NI ATLETICO NA REAL MADRID

CHELSEA imeaga Ligi ya Mabingwa Ulaya baada ya kufungwa mabao 3-1 na Atletico Madrid ya Hispania usiku huu Uwanja wa Stamford Bridge, London.
Atletico sasa itakutana na jirani zao, Real Madrid katika fainali mwezi ujao nchini Ureno, ambao jana waliwang’oa mabingwa watetezi, Bayern Munich kwa 4-0 mjini Munich na kufanya ushindi wa jumla wa 5-0.

Heshima sasa; Diego Costa kushoto akishangilia na mchezaji mwenzake, Koke baada ya kufunga bao la pili



Fernando Torres alitangulia kuifungia Chelsea dakika ya 36 kwa pasi ya Azpilicueta baada ya kazi nzuri ya Willian, lakini Adrian Lopez akaisawazishia Atletico dakika ya 44 kwa pasi ya Juanfran.
Diego Costa akafunga bao la pili kwa penalti dakika ya 61 kabla ya Arda Turan kumaliza kazi dakika ya 72 na Atletico imefuzu kwa ushindi wa jumla wa 3-1 baada ya sare ya 0-0 katika mchezo wa kwanza Madrid wiki iliyopita.
Mabadiliko yaliyofanywa na kocha Jose Mourinho dakika ya 54 kumtoa beki Ashley Cole na kumuingiza mshambuliaji Samuel Eto’o ndiyo yaliigharimu Chelsea. Eto’o ndiye aliyesababisha penalti iliyofungwa na Costa.

Wednesday, 30 April 2014

MAYWEATHER AONYESHA JEURI YA FEDHA, SASA ATAKA KUNUNUA TIMU MAREKANI

KAMA anavyotamba katika ngumi za kulipwa hadi sasa akiwa hajapoteza pambano licha ya kupigana na mabondia wakali duniani, Floyd Mayweather anataka kununua klabu ya mpira wa kikapu Marekani, inayomilikiwa na milionea anayekabiliwa na kashfa ya ubaguzi.
Hakuna ajabu kwa mkali huyo wa kutupa mikono kwenye miili ya wenzake, anayekwenda kwa jina la utani Money Mayweather juu ya hilo, kwa sababu ana uwezo kifedha.
Floyd Jnr anataka kutoa dola za Kimarekani Milioni 40 ambazo ni sehemu tu ya pato lake la pambano la Jumamosi wiki hii, atakalolipwa dola bilioni 1.8 ili kuinunua Los Angeles Clippers.
Mutu ya fweza: Floyd Mayweather akiwasili ukumbi wa MGM Grand kuelekea pambano lake na Marcos Maidana

Kuhusu Marcos Maidana, Muargentina anayetarajiwa kupambana naye mjini Las Vegas, Mayweather amesema: "Amekuwa babu kubwa katika mapambano yake manne yaliyopita. Ana wastani wa asilimia 80 ya Knockout (KO). Hivyo siwezi kumdharau huyu jamaa,".
Kuhusu Clippers, ambayo mmiliki wake Donald Sterling amefungiwa maisha kujihusisha na masuala ya mpira wa kikapu baada ya kupatikana na hatia ya kuwatolea maneno ya kibaguzi watu weusi wa timu yake wakiwemo wachezaji, Mayweather amesema: "Ninataka kuinunua Clippers? Ndiyo. Naweza kuwaunganisha pamoja watu ambao watakuwa tayari.
"Kununua timu ya Ligi Kuu ya kikapu ni kitu fulani ambacho nataka kuongeza katika kampuni yetu inayokua kwa kasi ya Mayweather Promotions, ambayo sasa si kwa ajili ya ngumi tu, bali tunajihusisha pia na mavazi, muziki na sinema,"alisema.


Kifungo cha maisha: Mmiliki wa Los Angeles Clippers, Donald Sterling hawezi kujihusisha na masuala ya mpira wa kikapu baada ya kutoa kauli ya kibaguzi hadharani

KATIBU MKUU WA FIFA AWASILI KESHO DAR

KATIBU Mkuu wa Shirikisho la Soka la Kimataifa (FIFA), Jerome Valcke anawasili nchini kesho (Mei 1 mwaka huu) ambapo atafungua semina ya mawasiliano kwa nchi wanachama wa Baraza la Vyama vya Mpira wa Miguu Afrika Mashariki na Kati (CECAFA).

Valcke ambaye atafuatana na maofisa wengine saba wa FIFA baadaye kesho hiyo hiyo (Mei 1 mwaka huu) atakuwa na mkutano na waandishi wa habari. Mkutano huo utafanyika saa 4 kamili asubuhi kwenye hoteli ya Double Tree by Hilton iliyopo Oysterbay, Dar es Salaam.

Sunday, 27 April 2014

MADOGO WA NGORONGORO WALIVYOWATOA WAKENYA JANA NA KUJIWEKA KWA NIGERIA


Kiungo wa timu ya taifa ya vijana ya Tanzania chini ya umri wa miaka 20, Ngorongoro Heroes, Mudathir Yahya akimtoka kiungo wa Kenya katika mchezo wa jana kuwania tiketi ya Fainali za Afrika nchini Senegal mwakani. Tanzania iliitoa Kenya kwa penalti 4-3 baada ya sare ya jumla ya 0-0. Ngorongoro sasa itamenyana na Nigeria katika hatua inayofuata.


Kevin Friday wa Tanzania akimuacha chini beki wa Kenya

Wachezaji wa Tanzania wakishangilia baada ya mechi


Ally Bilal wa Tanzania akimtoka Hillary Dan wa Kenya


Mange Chagula wa Tanzania kushoto akigombea mpira na Hillary Dan wa Kenya aliye tayari kusaidiwa na wenzake


Kipa wa Kenya, Farouk Shikhalo akidaka mpira huku akilindwa na beki wake, Hillary Dan aliye mbele ya Ally Bilal wa Tanzania

Kevin Friday wa Tanzania kulia akimtoka Victor Ndinya wa Kenya

Mange Chagula wa Tanzania akiteleza na mpira mbele ya Evans Makari wa Kenya

Iddi Suleiman wa Tanzania akiwatoka mabeki wa Kenya

Iddi Suleiman wa Tanzania akimuacha chini beki wa Kenya

Benchi la Ufundi la Tanzania wakati wa penalti jana

Thursday, 24 April 2014

REAL MADRID NA BAYERN MUNICH KATIKA PICHA JANA BERNABEU


Juu kwa juu: Cristiano Ronaldo (katikati) akiwa ameruka juu zaidi ya Alaba (wa pili kushoto) na Dante kuwania mpira wa juu katika Nusu Fainali ya kwanza ya Ligi ya Mabingwa Ulaya jana Uwanja wa Bernabeu mjini Madrid, Hispania. Real ilishinda 1-0.
Franck Ribery wa Bayern Munich (kushoto) akimfukuzia Daniel Carvajal wa Real
Mfungaji wa bao pekee la Real, Karim Benzema akishangilia baada ya kufunga Uwanja wa Santiago Bernabeu
Kula gwala, kamalizie kazi: Ronaldo akimpisha Gareth Bale dakika ya 74
Philipp Lahm na Gareth Bale (kulia wakigombea mpira wa juu
Beki Mbrazil wa Bayern, Dante (kushoto) akipitia mpira miguuni mwa Angel di Maria wa Real
Thomas Muller (katikati) wa Bayern akililia penalti
Beki wa Real Madrid, Sergio Ramos (kushoto) akiosha mbele ya mshambuliaji wa Bayern, Bastian Schweinsteiger
Schweinsteiger akimdhibiti kiungo wa Real Madrid, Xabi Alonso (katikati)
Mabeki wa Real, Pepe (kushoto) na Sergio Ramos (katikati) wakienda hewani kuondosha hatarini mpira wa juu kutoka kwa Ribery



Kipa wa Real, Iker Casillas (kulia) akiokoa mpira kichwani kwa Javier Martinez
Cristiano Ronaldo akimtoka Jerome Boateng

TARIMBA: NINA DHAMIRA YA KURUDI KUONGOZA YANGA SC

Na Amran Muhina, Dar es Salaam
RAIS wa zamani wa klabu ya Yanga SC ya Dar es Salaam, Tarimba Abbas amesema kwamba ana dhamira ya kurudi kuiongoza klabu hiyo, katika uchaguzi ujao uliopangwa kufanyika Juni 15, mwaka huu.
Tarimba ameiambia BIN ZUBEIRY jana kwamba, kwa sasa bado mapema mno kuzungumzia jambo hilo ingawa kama mwana-Yanga ana haki yake kikatiba.
“Ni mapema mno kusema nitagombea, maana uchaguzi ni mpaka Juni ni kipindi kirefu sana, lakini kama mwana-Yanga dhamira ninayo ingawa inaweza isiwe sasa, ila ninachoweza kusema ni mapema mno kuzungumzia jambo hilo,” alisema Tarimba.


Tarimba kulia akizungumzia pembeni ya Mkurugenzi wa Masoko wa Vodacom, Kevin Twissa

Tarimba ambaye kwa sasa ni kada wa CCM, Diwani wa Kata ya na Mkurugenzi wa Tume ya Michezo ya Kubahatisha ni kati ya watu ambao wana Yanga SC wanawataka sana waingie kuongoza klabu hiyo pamoja na Davis Mosha.
Angu Shadrack na wanachama wenzake vijana wa Kariakoo wanajipanga kumfuata Davis Mosha kumshawishi achukue fomu za kugombea nafasi ya Makamu Mwenyekiti, wakati Tarimba Abbas wanataka awania Uenyekiti wa klabu hiyo.
“Tunajipanga kuwafuata Mosha na Tarimba kuwaomba wagombee, hawa viongozi wetu wa sasa wametuangusha sana, tunataka watu ambao hatutawajaribu, tunajua ni watu wa kazi na wana mapenzi na Yanga,”alisema Angu.
Gazeti la Spoti Leo la leo nalo limewanukuu wanachama wa Yanga wakisema wanaamini Tarimba anastahili kuvaa viatu vya Manji kutokana na uwezo mkubwa aliouonyesha wakati akiwa Rais wa Yanga mwanzoni mwa miaka ya 2000.
“Tumeshakaa mara kadhaa wana-Yanga kujadili nani anafaa kuongoza baada ya Manji kumaliza muda wake, lakini wengi mawazo yetu yameangukia kwa Tarimba. Tunaamini ni kiongozi mzuri na anaweza kuipeleka Yanga pazuri,” alisema Juma Mohammed ‘Kamanda’ aliyejitambulisha anatoka Yanga Bomba.
Naye mwanachama mwingine wa Yanga, Suleiman Mussa, alisema wameanza mikakati ya kuangalia nani atafaa kuiongoza Yanga na wanajipanga kwenda kumuona Tarimba ili kumshawishi wakati ukifika ajitose kwenye uchaguzi huo.

Wednesday, 23 April 2014

DIEGO COSTA AWAPA ISHARA NZURI CHELSEA...NI DALILI ZA KUHAMIA DARAJANI

MSHAMBULIAJI wa Atletico Madrid, Diego Costa anaweza kuwa katika jaribio la kuing'oa Chelsea katika Ligi ya Mabingwa Ulaya, lakini alikuwa mwenye furaha kupita kiasi wakati anawapungia mkono mashabiki wa timu hiyo baada ya mechi ya jana.
Inafahamika mshambuliaji huyo ni chaguo la kwanza la kocha Jose Mourinho katika orodha ya wachezaji anaotaka kuwasajili msimu ujao na kitendo cha kuwapungia kwa furaha mashabiki wa Chelsea jana kimezidi kuongeza dalili za kuhamia kwake London.
Chelsea ilitoka sare ya bila kufungana na Atletico Madrid Uwanja wa Vicente Calderon, inamaanisha mchezo bado upo kati kwa kati kuelekea mechi ya marudiano Jumatano ijayo.

Anawapa dalili? Diego Costa akiwapungia mkono mashabiki wa Chelsea baada ya mechi usiku wa jana

Upinzani: Mshambuliaji huyo anaweza kuja kuwa mchezaji mwenzake John Terry msimu ujao, japokuwa jana walizinguana sana uwanjani
Baada ya filimbi ya mwisho mashabiki wa Chelsea walibaki uwanjani wakati baadhi ya wachezaji wanapita mbele yao kuondoka.

REAL HATARINI KUWAKOSA GARETH BALE NA RONALDO LEO DHIDI YA BAYERN, WOTE WAGONJWA

WINGA Gareth Bale yuko shakani kuichezaea Real Madrid katika Nusu Fainali ya Kwanza ya Ligi ya Mabingwa Ulaya dhidi ya mabingwa wa Ujerumani, Bayern Munich kutokana na kusumbuliwa nugonjwa wa mafua.
Nyota huyo wa Wales hajasafiri na wenzake kwa ajili ya mchezo wa kwanza leo Uwanja wa Sangtiago Bernabeu.
Kocha wa Real Madrid, Carlo Ancelotti pia anatilia shaka uzima wa Cristano Ronaldo. Nyota huyo wa Ureno anatarajiwa kufanyiwa vipimo vya afya muda mfupi kabla ya mchezo wa leo.

Shaka tupu: Gareth Bale anasumbuliwa na mafua kuelekea mchezo wa leo dhidi ya Bayern Munich

Pigo: Madrid inaweza kumkosa Bale na Cristiano Ronaldo leo
Ikiwa Bale ataukosa mchezo wa leo, litakuwa pigo kwa Ancelotti, ambaye alimwagia sifa nyingi winga huyo katika Mkutano na Waandishi wa Habari kuelekea mchezo wa leo.
Bale anang'ara kwa sasa, baada ya kufunga bao la ushindi katika fainali ya Copa del Rey dhidi ya Barcelona wiki iliyopita na kocha wake akasema mchezaji huyo aliyesajiliwa kwa Pauni Milioni 86 kutoka Tottenham atakuwsa mkali zaidi msimu ujao Hispania ambao utakuwa wa pili kwake Real.
"Gareth ni mtoto mkali,"alisema Ancelotti. "Anavutia kwa kujiamini kiasi cha kutosha hususan kutokana na bao alilofunga dhidi ya Barcelona katika fainali,"alisema.

Friday, 18 April 2014

BARCELONA SASA RADHI KUMUUZA MESSI

MSHAMBULIAJI Lionel Messi anaamini Barcelona sasa inamchukulia kama mtu wa kuuzwa na si tena nyota asiyegusika katika kikosi chao, imeripotiwa chaneli ya Televisheni ya Esport3 ya Katalunya.
Kusuasua kwa mazungumzo ya kuongeza mkatab baina ya mchezaji huyo na klabu ni kielelezo cha kwa nini Messi anafikiria muda wake umekwisha Barcelona.
Inaelezwa kwamba Wajumbe wa bodi wanaamini mchezaji huyo ana thamani zaidi ya kuuzwa kwa sasa kuliko kuendelea kuwatumikia uwanjani, jambo ambalo Messi analitambua pia na anaamini ni juu ya Barcelona kuhusu Mkataba wake unaomalizika mwaka 2018.

Mwisho? Lionel Messi anaweza kuondoka Barcelona kutokana na kusuasua kwa mazungumzo ya Mkataba mpya
Paris Saint-Germain inaweza kuwa tayari kumlipa mchezaji huyo mshahara wa Pauni Milioni 205, na kutokana na mpango wa ujenzi wa Uwanja mpya unaoweza kuigharimu Barcelona Pauni Milioni 493, inawezekana klabu hiyo ikafanya uamuzi usiofikirika na kumuuza mchezaji huyo ambaye amekuwa Barcelona tangu ana umri wa miaka 13.
Messi anataka kubaki Barcelona hadi atakapofikiri wakati wa kurejea klabu yake ya kwanza, Newell’s Old Boys ya Argentina umewadia, lakini Barcelona inaweza kumuuza kwa klabu nyingine ya Ulaya kati ya PSG hata Manchester City.


Babu kubwa duniani: Messi akiwa na tuzo ya Ballon d'Or ya mwaka 2012
MAFANIKIO YA LIONEL MESSI BARCELONA
2004:Mechi 420 mabao 351
La Liga 2004-5, 2005-6, 2008-9, 2009-10, 2010-11, 2012-13
Kombe la Mfalme: 2009, 2012
Ligi ya Mabingwa 2006, 2009, 2011
Rais wa sasa wa Barcelona, Josep Bartomeu alitaka kumpa mkataba mpya Messi kabla ya Fainali za Kombe la Dunia, lakini mchezaji huyo inafahamika anataka malipo ya Pauni Milioni 20.5 kwa mwaka na klabu inataka nusu ya haki ya matumizi ya picha zake, wakati kwa sasa mchezaji huyo anamiliki haki zote.
Kushindwa kuonyesha kiwango kilichotarajiwa katika Robo Fainali ya Ligi ya Mabingwa Ulaya na fainali ya Kombe la Mfalme kwa mara ya kwanza vimeifanya bodi ifikirie uamuzi wa kumpiga bei.